BODABODA WANAVYOITIA HASARA HOSPITALI YA BUGANDO

Hospitali ya Rufaa ya Bugando iliyopo jijini Mwanza.

HOSPITALI ya rufaa ya Bugando iliyopo jijini Mwanza imekuwa ikipata hasara ya takribani Sh. milioni tano mpaka milioni 12 kila wiki ikiwa ni misamaha ya gharama za matibabu ya majeruhi wa ajali za barabarani hususani bodaboda.

Katika mahojiano maalumu na mwandishi, Afisa Ustawi wa Jamii hospitali ya Bugando, Daudi Makumucha, alisema, “Gharama kubwa za matibabu zinawatesa majeruhi wengi wanofikishwa hospitalini.

“Wapo wanaolazimika kuuza mali zao ili aweza kumudu gharama za matibabu.”
Alisema hali hiyo inailazimu hospitali hiyo kutoa msamaha wa matibabu kila wiki kwa wagonjwa ambao hawana uwezo wala ndugu wa kumudu kulipa gharama hizo.

“Leo pekee (Julai 13, 2017) tumejadili mafaili ya wagonjwa kumi na kupitisha msamaha wa madeni kiasi kinachofikia shilingi milioni tano,….kuna mgonjwa kutoka wodi ya mifupa, alipata ajali na alikuwa anadaiwa takribani Sh. 2,474,800/-” alisema.

Kwa mujibu wa Makumucha, majeruhi hao mara nyingi hupata majeraha makubwa na kuwachukua muda mrefu kukaa hospitali hususan katika kitengo cha uangalizi maalum (ICU).

Mara zingine majeruhi hufikishwa bila kujitambua, lakini hospitali humtibia mpaka akizinduka ndipo ndugu zake hutafutwa.

Anaeleza kuwa wapo wagonjwa ambao hutoroka ili kukwepa gharama za matibabu. Hivyo hospitali kwa jumla hupoteza Sh. milioni tano mpaka 12, ambapo kwa mwezi inapoteza kati ya Sh. milioni 20 mpaka 48.

Kwa mwaka ikiwa ni kati ya takribani shilingi milioni 240 mpaka milioni 570, kutokana na msamaha wa madeni ya matibabu kwa majeruhi wa ajali za bodaboda peke yake.

Daktari bingwa wa mifupa katika hospitali ya Bugando, Dk. Isidor Ngayomela, alisema kuwa wanapokea majeruhi wa mifupa watatu mpaka wanne kila siku kutokana na ajali za barabarani. 
Kutokana na changamoto ya gharama za matibabu kuwa kubwa, elimu ya bima ni muhimu kutolewa ili wananchi wengi wajiunge na mifuko mbalimbali ya bima itakayowasaidia kujilinda dhidi ya majanga ya ajali kwa kupatiwa matibabu kwa unafuu zaidi.

Comments

Popular posts from this blog

AJALI ZA BODA BODA

Boda boda;Kundi linaloonekana kuwa sugu kwa kutofuata sheria za usalama barabarani